ads

VITA VYA BADR


UTANGULIZI

      Namshukuru m/mungu kwa kunineemesha neema hii na kunipa umri hadi leo hii bado ninaendelea katika kuitetea dini ya Allah (sw) ninamtakia ziada ya rehma mtume Muhammad (saw) na jamaa zake na waislam wanaume na waislam wanawake                   

      Baada ya kumshukuru Allah na kumtakia ziada ya rehma mtume Muhammad (saw). Hakika Allah leo hii amenipa nguvu ya kuwaelimisha waislam wenzangu juu ya suala zima la historia katika uislam na pia leo hii nitaelezea juu ya vita vya kiislam alivyopingana mtume (saw) na maswahaba zake na kuwapiga makuraishi ambavyo viliitwa vita vya badr                             
                                                                                                                                                                       VITA VYA BADR

      Badr ni jina la mji uliopo kiasi cha kilomita mia na hamsini(km150) mbali na mji wa madina na mahali hapo hapakuwa na chochote isipokuwa bonde na kisima kilichokuwa milki ya mtu mmoja aitwae Badr na kwa ajili hiyo mahala hapa pakaitwa badr, kwa vile vita hivyo vilipiganwa mahali hapa ndiyo maana vikaitwa vita vya badr

      Vita hivyo vilitokea asubuhi ya siku ijumaa Ramadhani ya kumi na saba mwaka wa pili baada ya hijra (baada ya mtume (saw) kuhamia madina)


SABABU ZA VITA

       Chanzo cha vita hivi kilikuwa ni msafara wa biashara wa makafiri ukiongozwa na            abu sufyan uliokuwa ukitokea nchi ya sham (Syria) ukirudi makkah ukiwa na watu wasiozidi Arobaini (40)

       Msafara huu ulikuwa umebeba mali nyingi sana ya watu wa makkah na mtume (saw) akaona hii ndiyo fursa nzuri ya kuipiga dola hiyo ya kikafiri kiuchumi, kijeshi na kisiasa na pia kulipiza kisasi hasa kwa vile waislam walipohama makkah kwenda madina makafiri waliwalazimisha kuziacha mali zao zote huko, na kuondoka bila chochote isipokuwa nguo zao na wanyama wa kuwapanda hata hivyo wengine walinyang’anywa wanyama wao na ikabidi kutembea kwa miguu mpaka madina na wengine waliviziwa njiani na kuuliwa

        Mtume(saw) pia akawaambia waislam”msafara huu wa makurashi umejaa mali zao, uendeeni huenda Allah akatulipa haki zetu walizotunyang’anya kwa kutuwezesha kuuteka”

Si watu wengi waliojitolea kwenda, na hii ni kwa sababu mtume (saw) hakutia mkazo katika suala hili na akawaachia watu wajitolee wenyewe bila ya kulazimishwa na kwa ajili hiyo maswahaba wachache tu walimfuata 


NGUVU YA JESHI LA KIISLAM

           Mtume (saw) akaondoka na watu wapatao mia tatu na kigodo tu hivi, inasemekana walikua mia tatu na kumi na tatu( 313) na riwaya nyengine zinasema walikuwa mia tatu kumi na saba (317), themanini na sita (86) ni muhajirina na mia mbili thelathini na moja (231) ni watu wa pale pale

           Maswahaba hawakujuwa kuwa msafara huo utakuja kuwa ni moja ya mapambano makubwa baina ya haki na batili walidhani kuwa yatakuwa yale mapambano ya kawaida na wapiganaji wadogo wadogo tu na wala hawakujuwa kuwa Allah amekwisha panga atimize jambo lililokuwa lazima litendeke, Waliondoka wakiwa na farasi wawili tu, mmoja wa zubeir bin Awaam na mwengine wa mikidadi bin Al-Aswad Al-kindly(ra) walikuwa pia na ngamia sabiini wakipokezana katika kuwapanda

Msafara wa Abu sufyan

        Abu sufyan alikuwa kiongozi wa msafara wa biashara ya makafiri wa makkah alikuwa ni mtu mwenye kuchukuwa tahadhari sana, alijuwa kuwa njia ya makkah ina hatari nyingi na kwa ajili hiyo kila mara alikuwa akitanguliza wapelelezi ili wamletee habari za mbele safari wakati huo huo alikuwa akimuuliza kila anayekutana naye, iwapo huko alikotoka  ameona chochote kile kisichokuwa cha kawaida, katika kuuliza uliza akamuuliza mtu mmoja aitwae Majdi bin Amru iwapo ameona jeshi kutoka mji wa madina akasema “mimi sikuona majeshi lakini niliona kundi kubwa la watu waliopumzisha ngamia wao mahali hapa”

        Abu sufyan akaenda kupafanyia uchunguzi mahali pale alipoambiwa kuwa watu walipumzisha ngamia wao, baada ya kuchambua kinyesi cha ngamia waliopumzishwa mahali hapa na kuona kokwa za tende za ndani yake akasema”maadam choo chao kimejaa kokwa za tende bila shaka yoyote kuwa hawa ni ngamia wa watu madina“

         Alipotambuwa hayo akajua kuwa anaviziwa na hapo hapo akageuza msafara na kupita njia nyengine na akamtuma mtu mmoja aitwae Dhamdham bin Amru Al-Ghafariy atngulie mbio sana aende akawazindue watu wa makkah juu ya hatari inayoukabili msafara wao wenye vitu vya thamani kubwa sana, Watu wa makkah walipoyasikia  haya wakasema”Muhammad anadhani kuwa atauteka msafara huu kwa urahisi kama alivyouteka msafara wa Amru bin Al-hadhramy” akaendelea kusema “haitakuwa hivyo kabisa atakiona cha moto chake Muhammad safari hii”


Jeshi la makafiri wa makkah

        Makafiri mara baada ya kujulishwa juu ya hatari hiyo wakakusanya jeshi la watu wapatao elfu moja na mia tatu (1300), farasi wapatao mia moja (100) na ngamia wengi sana. Wakaondoka pamoja na vigogo vya makuraish na walisafiri kwa kasi kubwa sana kuelekea kaskazini mahali ulipo mji wa badr,walipofika mji uitwao Al-juhufa wakapata salamu kutoka kwa Abu sufyan kuwa umekwisha salimika msafara wao na kuwataka warudi makkah

         Abu jahal akasema haturudi mpaka tufike badr, tukae hapo siku tatu tuchinje wanyama wetu, tunywe pombe zetu na waimbaji waimbe mpaka habari zetu ziwafikie waarabu wote ili wapate kutujua ni nani sisi na ili watuogope 


Mtume (saw)ashauriana na sahaba zake

          Kutokana na mabadiliko haya ya ghafla na ya hatari ilimbidi mtume(saw) awaite wakuu wa  jeshi la waislam ili kuwajulisha juu ya hali ya mambo ilivyo na kutaka ushauri wao.

          Ama wa kwanza wao ni Abu bakar (ra) akamuunga mkono mtume(saw) juu ya kulazimika kwao kupigana na makafiri, kisha akasimama Umar (ra) naye akamuunga mkono mtume kwa rai yake, kisha Amru (ra) akasema “Ewe mtume wa Allah nenda kama alivyokuonyesha Allah na sisi tuko nyuma yako wallahi hatutakuambia kama walivyo mwambia wana wa israili mtume wao Mussa(as); nenda wewe na mola wako mkapigane nasisi tutakaa hapa tunawangojea; Bali tunakwambia nenda wewe na mola wako na sisi pamoja nanyi tunapingana”. Baada ya maneno haya mtume (saw) akasema”vyema”. Kisha akawaombea dua wote watatu waliotoa rai zao kwa upande wa muhajirina na kwa upande wa madina akasimama sa’ad bin mua’adh(ra) aliyekuwa mmoja wa viongozi wa watu wa madina aksema “sisi tumekuamini na kukusadiki na tukashuhudia kuwa uliyokuja nayo ndiyo ya haki na tukakupa ahadi zetu na neno letu kuwa tutakusikiliza na kukutii kwa hiyo endelea tu kama unavyotaka kwani wallahi kama utatutaka tuivuke bahari hii,ukaivuka basi tutaivuka pamoja nawe na hapana hata mmoja kati yetu atakaebaki nyuma sisi hatuogopi kupambana na adui kesho, sisi ni watu wenye kusubiri katika vita na wakweli katika mapambano na inshaallah Allah atkuonyesha ndani yetu yale yatakayo kufurahisha macho yako, kwa hiyo tuongoze kwa baraka za Allah”

            Mtume (saw) akafurahishwa na maneno ya sa’ad (ra) akasema “nendeni na nakupeni bishara njema, Allah ameniahidi moja wapo ya makundi mawili wallahi kama kwamba ninaona wapi wataanguka kila mmoja kati ya maadui”
 
map of badr land

Majeshi ya kiislam yanafanya upelelezi

             Walipowasili mahali panapoitwa Addiya karibu na badr, mtume (saw) pamoja na swahiba yake wa pangoni Abu bakar As-swidiq (ra) wakatoka na kuanza kufanya upelelezi nje ya kambi yao na katika kutembea kwao, wakakutana na mzee mmoja wa kiarabu na kumuuliza juu ya habari za jeshi la makuraishi na juu ya habari za jeshi la Muhammad (saw), ili asiweze kumtambua ni katika kundi gani wao, Yule akamwabia”kabla sijakujibu niambieni kwanza nyinyi mnatokea wapi?”. Mtume (saw) akamwabia “ukituambia nasi tutakwambia”  Yule mtu akasema “nilisikia kuwa jeshi la Muhammad na swahiba zake lilitoka siku kadhaa wa kadhaa, ikiwa habari hizi ni za kweli, basi leo watakuwa washafika mahali kadhaa, akapataja mahali lilipojeshi la watu wa madina, na nimesikia kuwa makuraysh wametoka siku kadhaa wa kadhaa na ikiwa maneno niliyoambiwa ni kweli, basi leo watakuwa washafika mahali kadhaa wa kadhaa, akapataja mahali lilipojeshi la watu wa makkah”

           Baada ya kumaliza maneno haya akawauliza “nyinyi mnatoka wapi?”. Mtume akamwambia “sisi tunatokana na maji” kisha akaondoka. Yule mtu akawa anajiuliza “hawa wana katika maji ya iraaq au maji gani?

            Na ifahamike kuwa mtume hakusema uongo, kwani viumbe vyote vinatokana na maji, Allah anasema “na tukafanya kwa maji kila kitu kilichohai” (suratul anbiyaa aya 30)

           Mchana wa siku hiyo, mtume (saw) aliwatuma watu watatu kwenda kupeleleza juu ya habari za jeshi la makuraishi nao ni Ally bin Abi Talib, Az-zuberybin Awaam na Sa’ad bin Abi waqas(ra) walipokwenda penye visima vya badr wakawakuta watoto watatu wanachota maji kwa ajili ya kuwapelekea jeshi la makuraishi, wakawateka na kwenda nao kambini ili kuwauliza maswali, walipofika nao kambi, Mtume alikuwa akiswali, kwa hiyo wao wakaanza kuwauliza mateka wao. Vijana hao wakasema wametumwa na makuraishi ili kuwachotea maji, maswahaba walikasirishwa na jibu hilo kwani wao walitamani wawe watu wa Abu sufyan. Wakawapiga wale vijana mpaka wakasema kuwa wao ni watu wa Abu sufyan na si watu wa jeshi la makuraishi

          Mtume  baada ya kumaliza swala akawaambia maswahaba”waliposema kweli mliwapiga na walipokudanganyeni mkawachilia, walisema kweli wallahi kwani wao ni watu wa jeshi la makuraishi”. Kisha mtume akawauliza wale vijana “nipeni habari za makuraishi ”, wakasema wapo katika ng’ambo ya bonde lile la mbali, akawauliza “wako wangapi”. Wakasema” wengi”. Akawauliza mtume “idadi yao ngapi”, wakasema hatujui. Akawauliza tena  wanachinja wanyama wangapi kila siku”, wakasema wale vijana “siku nyingine wanachinja ngamia tisa na siku nyingine kumi”. Mtume akasema kuwaambia maswahaba (ra) ”idadi yao ni baina ya watu mia tisa na elfu

           Mtume akawauliza tena wale vijana “nani katika vigogo vya makuraishi wamo miongoni mwao ”, wakasema “utbah na shaiba watoto wa Rabia, Abu Al-bakhtari bin hishaam, Hakiym bin Hizaam, Naufil bin Khuwaliid, Al-Haarith Taimah, An-nadhar bin haarith, Zaamah bin Aswad, Abu jahal bin hishaam na Umayyah bin khalaf”. Mtume akasema kuwaambia maswahaba zake (ra) “makkah imekutupieni (imekuleteeni) vipande vya maini yao (vigogo vyao na vipenzi vyao)” 


KUTEREMKA KWA MVUA

            Waislam wakasogea mpaka wakakaribia bonde la karibu na mahali yalipopiga kambi makuraisha na majeshi yao

           Allah aliwateremshia waislam utulivu wakalala vizuri hata wengine wakaota na kuamka wa kiwa na janaba, lakini mahali hapo hapakuwa na maji ya kogea ili wapate kujitwaharisha na wala ya kunywa na shaitwani akaanza kuwatiya wasiwasi “vipi mtapigana kesho wakati miili yenu haina twahara, vipi mtapigana kesho wakati mna kiu……?”

           Allah (sw) akawateremshia mvua iliyo wasaidia sana kwasababu kutokana na mvua hiyo waliweza kujitwaharisha na kuondoa uchafu wa sheitwani na kuzipa nguvu nyoyo zao na pia na pia yakawasaidia kuufanya mchanga chini yao uwe mgumu ili waweze kutembea vizuri bila ya kuteleza wakati wa mapambano.Allah anasema “alipokufunikeni kwa usingizi uwe ni uaminisho kutoka kwake na akakuteremshieni maji kutoka mbinguni ili kukusafisheni kwayo na kukuondoleeni uchafu wa sheitwani na kuzipa nguvu nyoyo zenu na kuitia imara miguu yenu” (suratul Anfaal:11)

            Mtume (saw) akaliamrisha jeshi lake liondoke pale walipo haraka sana ili wawahi kusogea mbele karibu na mahali yalipo maji ya mji wa badr, wakasogea mpaka wakafika mwanzo wa visima vya maji ya badr na mtume (saw) akawamrisha kupiga kambi hapo. Mmoja katika maswahaba aitwaye Al-khabaab bin Mundhir akamuuliza mtume(saw) “Ewe mtume wa Allah mahala hapa tulipo simama Allah amekuamrisha na hatuna haki ya kusonga mbele zaidi au katika hila za kivita tu na rai yako mwenyewe?” Mtume (saw) akamwambia “Bali ni hila za kivita na rai yangu mwenyewe” akasema Al-khabaab “Ewe mtume wa Allah mimi naona kuwa hapa si makazi mazuri bora tusogee mbele mpaka mwisho wa visima vya badr tuvizunguke kisha tujenge mahodhi tuyajaze maji kisha tupambane nao sisi tutakuwa tunakunywa na wao wasipate kunywa”. Mtume (saw) akasema “rai uliotoa ni nzuri”. Wakaondoka hapo na kusogea sehemu ya juu ya mahali yalipo maji na usiku wakaanza kutengeneza mahodhi na kuyajaza maji


MAKAO MAKUU YA JESHI LA WAISLAM

          Baada ya kumaliza kazi yao hiyo sa’ad bin Mu’aadh (ra) akatoa rai nyengine pajengwe mahali patakapo kuwa makao makuu ya jeshi lao ili waweze kujitayarisha na kuikabili hali ya hatari yoyote itakayo tokea iwapo jeshi lao litashindwa katika vita hivyo akasema “Ewe mtume wa Allah unonaje kukujengea kipaa mfano wa hema (Arshii), kisha tukakuwekea tayari wanyama wa kupanda kisha sisi tutapambana na adui ikiwa Allah atatujaalia kuwashinda hayo ndiyo tunayoyapenda, ama ikiwa kinyume na hivyo basi wewe utapanda wanyama wako na utakwenda kujiunga na wenzetu tuliowaacha nyuma kwani hao tuliowaacha nyuma mapenzi yao juu yako ni makubwa pia kama sisi wangelijuwa kuwa tunapambana na adui basi wasingelirudi nyuma kabisa na wangelipigana jihadi pamoja nawe”.   Mtume (saw) akamuombea kila la kheri kwa rai yake hiyo, na waislam wakajenga mfano wa hema juu ya kilima sehemu ya kaskazini ya uwanja wa mapambano, sehemu ambayo mtu anaweza kuviona vita bila tabu huku vikipiganwa.

           Usiku kabla ya mapambano, mtume (saw) alilipanga jeshi lake kisha akawa anawaonesha maswahaba(ra) mahali watakapo kufa maadui mbali mbali kabla hata vita havijaanza alikuwa akisema “hapa ataanguka Fulani, hapa atauliwa Fulani……”  

             Alipokuwa akiwapanga watu wake, mtume (saw) alipita mbele ya Sawaad bin Aziya (ra) akamgonga kwa nguvu tumboni kwake kwa bapa la mkuki na kumwambia “simama vizuri ewe Sawad”. sawad(ra) akamwambia mtume “umeniumiza ewe mtume wa Allah, na mola wako amekuleta kwa ajili ya kusimamisha haki na uadilifu, kwa hiyo uniache na mimi nikulipizie katika mwili wako”. Mtume (saw) akalifunuwa tumbo lake na kumwambia “ewe sawad jilipie kisasi chako”. Sawad akalikumbatia tumbo la mtume huku akilibusu, mtume (saw) akamwambia “kipi kilichokupeleka ukafanya hivi?”. Akasema sawad “Ewe mtume wa Allah mambo ndivyo kama unavyo yaona na mimi nilipenda tendo langu la mwisho kabla sijafa liwe ni kuugusa mwili wako”. Mtume (saw) akamuombea dua nzuri.

              Baada ya kuwapanga watu wake sawa na kuwataka wasianze kupigana mpaka atoe amri yake, akawaambia maswahaba “wakianza kuja anzeni kuwarushia mishale na msitoe panga zenu mpaka wawe karibu nanyi kabisa”
 
map of battle land

JESHI LA WATU WA MAKKAH

               Usiku ule baadhi ya makuraishi waijaribu kutaka kunywa maji penye mahodhi wliyoyajenga waislam kalini kila aliyejaribu kuyasogelea aliuliwa isipokuwa mtu mmoja aitwae Haakim bin Hizaam huyu aliachwa na alisilimu na baadaye akawa muislam mwema

               Makuraysh waimtuma Umair bin Wahaab Al-jahamiy aende kuchunguza nguvu za jeshi la waislam, akawa anazunguka jeshi hilo akiwa juu ya farasi wake, huku na kule kisha akarudi kwa wenzake na kuwaambia “jeshi lao ni kiasi cha watu mia tatu na zaidi kidogo, lakini naona kesho balaa litakuwa kubwa sana, kwani watu hawa hawana pakukimbilia na hawana cha kupoteza, wanajuwa kuwa wao watauliwa tu, hawana isipokuwa panga zao tu, na nyuma yao jangwa tupu kwa hiyo inaelekea watapigana kwa ushujaa zaidi na hawatokubali mmoja wao auliwe bila ya yeye naye kuuwa mtu mmoja kati yenu, kwa hiyo tizameni wenyewe”. Pakatokea mzozo mkubwa baina ya makuraysh, wengi wao wakamtaka Abu jahal arudi na jeshi lake makkah na kwamba hapakuwa na haja ya kupigana na jeshi la Muhammad (saw), lakini Abu jahal kwa haraka akafanikiwa kuuzima moto huo na kumlaumu Umair kwa kumwambia “umeingiwa na khofu wewe ulipouona uso wa Muhammad, pale ulipokuwa ukichunguza majeshi yake ndiyo sababu ukaja na uwoga na unataka kututia na sisi uwoga huo”. Akaweza kuwaingiza watu wake mori wa vita kwa kuwa kumbusha kuuliwa kwa Amru bin Al-hadhramy na kwamba lazima walipize kisasi





MAJESHI YANAPAMBANA

             Asubuhi ya siku ijumaa tarehe kumi na saba mwezi wa ramadhani, mwaka wa pili baada ya hijrah, majeshi hayo mawili yakapambana. Allah (sw) aliwafanya waislam walione jeshi la makafiri kuwa ni wachache ili wasiogope na akawafanya makafiri wawaone waislam pia kuwa ni wachache ili wasiwaogope na kurudi nyuma, yote haya ili kutendeke kile anachokitaka Allah (sw)

            Kwa kawaida kabla ya kuanza mapambano, waarabu walikuwa na tabia ya kuanzisha mubaraza, na maana yake ni mtu mmoja au wawili au watatu hutoka kutoka katika kila upande na kuanza kupambana wao kwanza, kila mmoja na mwenzake mpaka wauwane, kisha vita ndiyo vinaanza. Mapigano haya kwa kawaida ndiyo yanayotoa picha ndogo ya mwisho wa vita

            Katika mapigano haya mtume (saw) aliwatoa upande wa waislam Ali bin Abi Talib, Ubaidah bin Haarith na Hamza (ra). Kwa upande wa makafiri wakatoka Utbah na ndugu yake Shaibah na Al-waliid motto wa Utbah. Wote wakiwa watu wa aina mmoja katika mapigano haya, Hamza alimuuwa mpinzani wake Shaibah na Ali (ra) alimuuwa mpinzani wake Al-waliid bila tabu na bila ya kuchukuwa muda mrefu, ama Ubaidah (ra) yeye na mpinzani wake wote waliumizana wakaanguka chini lakini Ali na Hamza wakawahi kumrukia Utbah na kumuuwa kisha wakamuokowa mwenzao na kumvuta nyuma na kumrudisha katika kambi ya waislam. Lakini hatimaye kutokana na damu nyingi iliyomwagika alifariki dunia siku nne baada ya tukio la badr kwa homa ya manjano.


MASHAMBULIO

           Majeshi yalipoanza kupambana mtume(saw) akaingia ndani ya lile hema yeye na Abu bakar (ra) peke yao na hapana mwengine aliyeingia humo, Mtume(saw) akaanza kuomba dua huku akisema “mola wangu hawa makuraishi wamekuja kwa jeuri na kiburi chao, wakikupinga na kumkadhibisha mtume wako, mola wangu nitimizie yale uliyoniahidi, mola wangu watu hawa wakishindwa leo, basi hautaabudiwa tena……” kila vita vikipamba moto, naye huongeza kuomba dua, akawa anaendelea kuomba mpaka nguo yake ya begani ikamwanguka na Abu bakar (ra) akaiokota na kumvisha tena huku akimwambia “inatosha ewe mtume wa Allah ushamuomba vya kutosha mola wako”. Kisha mtume(saw) akasimama penye mlango wa hema aliyojengewa akawa anaisoma aya ya 45 ya suratul Qamar “Wingi wao huo karibuni watashindwa na wataendeshwa mbio na watageuza migongo”

           Mapigano haya yalimaanisha mwisho mbaya wa jeshi la washirikina kwa sababu wamepoteza watatu katika wapiganaji wao wakubwa kwa mpigo mmoja, kwa ajili hiyo wakawavamia waislam kwa ghadhabu na kwa nguvu zao zote na waislam wakapambana nao kwa ujasiri mkubwa kabisa.

          

           Wakati huo mtume (saw) akawatokea waislam na kuwaambia “Naapa kwa Yule  ambaye nafsi ya Muhammad (saw) ipo mikononi pake, yeyote atakayepigana nao leo, kisha akauliwa akiwa katika hali ya kusubiri (subra) bila ya kurudi nyuma basi Allah atamuingiza peponi”. Umair bin Al-hamaam (ra) aliyekuwa akila tende, mara baada ya kusikia maneno hayo akasema “Hivyo baina yangu na baina ya kuingia peponi ni kupigana na kuuliwa na watu hawa na tende hii ndiyo inayonicherewasha” akazitupa tende zake akaingia vitani akapigana mpaka akauliwa

             Mtume (saw) akasogea mbele akachota gao la mchango, akawakabili makuraishi kisha akasema “zimeangamia nyuso zao”. Allah anasema “hamkuuwa nyinyi Allah ndiye aliyewauwa na wewe hukutupa pale ulipatupa, walakini Allah ndiye aliyetupa ili awajaribu waumini majaribio mema yatokayo kwake hakika  Allah ndiye msikizi na mjuzi ndiyo hivyo na hakika Allah ni mwenye kudhoofisha vitimbi vya makafiri” (suratul Anfaal:17-18).

             Kisha mtume (saw) akawaambia swahaba zake (ra) “wakazieni vizuri, inukeni muifuate pepo ambayo upana wake tu ni sawa na mbingu na ardhi” kisha akaondoka na kurudi katika hema lile alilojengewa. Mapambano makali yakaanza baina ya makundi mawili hayo, na ushindi ukawa wa waislam, wakauliwa waliouliwa katika vigogo vya makuraishi na wakatekwa waliotekwa, haya ni mapambano ya pekee ambayo malaika walishiriki, akiwemo jibril(as). Baadhi ya maswahaba walisema “siku hiyo tulikuwa tunaona vichwa tu na kuruka huku na kule, hatujuwi nani anayevikata” 


KIFO CHA ABU JAHAL

              Abu jahal alipoona majeshi yake yanaanza kurudi nyuma akawa anapiga kelele huku akisema “wasikutisheni hao,msiogope kwa kuwa Utbah na Al-waliid wameuliwa, leo hatuondoki hapa mpaka turudi nao makkah tukiwa tumewafunga kamba wote hawa”

              Anasema Abdulrahman bin Auf kuwa “nilipokuwa nimesimama vitani nikageuka kutizama kuliani kwangu na kushotoni nikidhani watakuwepo watu wazima ili tusaidiane vita vikipamba moto, lakini nikavunjika moyo nilipowaona watoto wawili wadogo wamesimama mmoja kushotoni pangu na mwengine kuliani pangu, nikasema moyoni mwangu “leo sina pakuegemea”, Yule mtoto aliye kuliani pangu akaiomba niiname apate kuniuliza ili yule mwenzake asisikie. Akaniuliza “Ami! Yupi kati yao Abu jahal?”  nikamuuliza “Ewe mwana wa ndugu yangu unamtakia nini Abu jahal?” Akanijibu “nimemsikia kuwa anamtukana mtume wa Allah, wallahi nikimuona basi sitomwacha, lazima nitamuuwa”, Yule mtoto aliye kushotoni pangu akaniuliza vilevile kama mwenzake na nikamjibu kama mwenzake na akasema yale yale aliyosema mwenzake; nilipomuona Abu jahal nikawaambia “Yule rafiki yenu mnayemtafuta”, Wakamkimbilia na panga zao wakamvamia na kumpiga kwa mapanga mpaka wakamuuwa

            

              Mara baada ya kumuuwa wakakimbia mpaka kwa mtume (saw) na kumpa habari njema hizo, mtume (saw) akawauliza “yupi kati yenu aliyemuuwa”. Kila mmoja akasema “mimi ndiye niliyemuuwa”. Mtume (saw) akawaambia “hebu nione panga zenu”. Baada ya kuzitazama akasema “kweli, nyote mmeshirikiana katika kumuuwa”. Kisha akasema “Allahu laailaaha illa huwa” mara tatu, kisha akasema “Allhamdu lillahi lladhiy swadaq wa’adah wa naswara abdahu,wahazamal-ahazaba wah-dahu”

             Katikavita hivi waliuliwa makuraishi sabiin (70) na wengine sabiin(70) walitekwa, na katika waliouliwa alikuwemo firauni wa umma huu; Abu jahal na utbah bin Rabia na mwanawe Al-waliid na nduguye Shaiba na wengine wengi, na miongoni mwa mateka alikuwemo; Abbas (ami yake mtume {saw}) na Aqiyl bin Abi Talib na Nawfal bin Al-Haarith na Umayya bin khalaf na wengine wengi, hawa wote walikuwa upande wa makuraishi 
 

MIZOGA YA MAKAFIRI

              Baada ya vita kumalizika, waislam wakawazika wenzao waliokufa mashahidi na idadi yao walikuwa kumi na nne {14}, kisha wakaichukuwa mizoga ya mushirikina na kuitupa katika kisima kisichokuwa na maji kilicho karibu na mahali palipotokea mapambano hayo.

              Usiku wa manane waislam walimsikia mtume(saw) akiwa amesimama penye kile kisima walichotupa mizoga ya mushirikina akiwafokea huku akisema “Enyi mlio kisimani, ubaya ulioje mliokuwa nao jamaa zangu nyinyi kwa mtume wenu!, mlinikadhibisha wakanisadiki watu (wakweli), mkanitoa katika mji wangu, wakanipokea watu (wakweli), mkanipiga vita wakanisaidia watu (wakweli), je! Sasa nyinyi mmekwisha pata kweli yale aliyo kuahidini mola wenu? Ama mimi nimepata yale aliyoniahidi mola wangu” 

               Maswahaba wakamuuliza mtume(saw) “Ewe mtume wa Allah unazugumza na watu washakuwa mizoga”, mtume (saw) akasema “Wao wanasikia kuliko nyinyi haya niliyowaambia isipokuwa hawawezi kujibu

BISHARA NJEMA

               Mtume (saw) aliwatuma watu kwa haraka sana waende madiynah ili kuwapa habari njema hizo za ushindi wao juuu ya makafiri, Usamah bin zayd (ra) anasema “zilitufika habari tulipokuwa tukimzika bibi Ruqayya (ra) bint wa mtume (saw), mke wa Uthamin bin Affan (ra); Zayd bin harithah (ra) alipoingia msikitini watu walimzunguka huku akisema kwa furaha “Amekwisha uliwa Utbah bin Rabia na shaibah bin Rabia na Abu jahal…..” akawa anawataja mmoja mmoja katika vigogo vya makuraishi waliouliwa Badr

               Zayd bin Harithah (ra) anasema “nikamuuliza babangu unasema kweli?” akanijibu “Naam, kweli mwanangu”



KUONDOKA MJI WA BADR

            Mtume (saw) akaondoka hapo badr pamoja na mateka wao na ngawira zao na alipofika karibu na madinah alisimamisha msafara katika bonde la safra akawagawia waislam ngawira yao sawa sawa na kila anapoukaribia mji wa madinah, alikuta makundi kwa makundi ya watu waliosimama pembezoni mwa njia wakimpongeza.

            Allah anasema “kumbukeni pale mlipokuwa nyinyi kwenye ng’ambo ya karibu ya bonde,na wao wakawa ng’ambo ya mbali, na msafara ulipokuwa chini yenu. Na ingeli kuwa mmeagana mngeli khitalifiana katika miadi. Lakini (mkakutana) ili Allah atimize jambo liliokuwa lazima litendeke kwa sababu, aangamie wa kuangamia kwa dalili zilizo dhahiri, na asalimike wa kusalimika kwa dalili zilizo dhahiri, na Allah ni mwenye kusikia mwenye kujua, kumbuka alipo kuonyesha usingizini mwako kwamba wao ni wachache na lau angeli kuonyesha kuwa ni wengi, mngeli ingiwa na woga, na mngeli zozana katika jambo hilo, lakini Allah kakuvueni, hakika yeye ni mwenye kuyajua yalio vifuani”


 HITIMISHO

             Ama tumshukuru Allah kwa kutujaalia sisi na mtume wetu kupata ushindi dhidi ya makafiri na hii ndiyo ilikuwa vita ya kwanza kupigana na makafiri, Allah awalipe kila la kheri wote wanao isimamisha dini yake katika njia ya haki, na pia mshairi anasema juu ya neema za Allah (sw)        

                             Umeniumba insani, mwanadamu alo huru   

                         Ukanipa Qur-an, ili iwe yangu nuru

                         Sasa nina kheri gani, kama sijakushukuru

                         Kwa nini nisikupende, nawe umenikirimu   

Ama mpaka kufikia hapa hatuna budi kumshukura Allah kwa kutujaalia kuliendeleza jahazi hili la uislam kwa kujulishana habari zilizopita za uislam kuhusiana na historia ya vita vya kiislam ambavyo ni vita vya badr . pia endelea kusoma vitini hivi na hiki kikiwa ni sehemu ya kwanza  na  sehemu ya pili inafuata  ambayo itahusu historia ya vita vya Uhud , INSHAALLAH.



                          Wabillah tawfiq 

Post a Comment

0 Comments