ads

WARID KATIKA MSITU - Kisa Cha Nuur

Bismillahir-Rahmaanir-Raheem.Alhamdulillah




 Rabbil'alamiin.  Subhana Allaahi rabbil'arshil adheem. Hakika sifa njema zote ni za Allaah سبحانه وتعالى  tunamsifu na tunamuomba msaada na tuna muomba maghfira. Na tunamuomba atuhifadhi na shari za nafsi zetu, na maovu ya matendo yetu.  Anaemuongoza  Allaah سبحانه وتعالى hapana wakumpoteza na  Anaempoteza hapana wa kumuongoza.  Nakiri kwamba hapana apasae kuabudiwa illa Allaah سبحانه وتعالى, hali ya kuwa peke yake, hana mshirika, na ninakiri kwamba Muhammad ni mja wake na ni Mtume wake.  Mwenyeezi Mungu  amrehemu na awarehemu jamaa zake na masahaba zake na wanaofuata hao kwa wema mpaka  siku ya malipo na amsalimishe kwa amani nyingi.

Napenda nishirikiane nanyinyi  kisa cha safari yangu kufikia Uislamu dini ya  asili iliyo safi na ya haki kabisa Aliyotuletea Mola wetu kutuongoza katika njia iliyonyooka  kufuata kitabu chake na Mtume  wake wa mwisho. 
  


KABLA YA UISILAMU

Jamii, malezi na dini yangu

Nimezaliwa India katika jamii ya  Sikh (Singa Singa).  Nimekulia katika malezi ya mzazi mmoja tu ambaye ni mama yangu, baba yangu alitangulia zamani kuja Canada akituacha mimi na mama yangu na mdogo wangu wa kike.   Watu katika mujtamaa wangu ni watu washupavu, tabia zao nyingi ni mbaya na za uwongo, za kuhadaiana. Na matajiri ndio zaidi wenye tabia hizo, maskini ni mtu wa kupuuzwa na kudharauliwa, na hakuna kuwaonea huruma wala kuwasaidia, bali wanazidi kuwa katika hali hiyo. 

 Mama yangu alikuwa mkali sana na mshupavu. Alipata tabu kutulea kuhakikisha tunapata elimu nzuri pamoja na mafunzo mazito ya dini yetu ya Ki Singa Singa.   Mzunguko wa maisha yangu yalikuwa ya kidhiki kwa kukosa mapenzi ya wazazi wawili, kwa hiyo sikuwa katika hali   nzuri ya kisiha ya akili, kimwili hata ikawa imeniathiri hisia zangu. 

Nimesomeshwa katika shule bora kabisa ya dini yetu na mafundisho niliyopewa kuhusu mungu ni kuwa tuamini kwamba haifai kumuwaza mungu kwa kufuata akili za binaadamu, yaani hakuna nafasi ya hoja au busara katika jambo hilo.   Nakumbuka nilivyokuwa nikiwaza kuhusu mbingu na ardhi  na nilivyozaliwa na kuwaza moyoni, "kama vyote hivyo vimeumbwa, bila ya shaka kuna muumbaji wa hivi vyote.”  Nikimuuliza mama yangu, hakuwa ananipa jibu lolote bali kuniambia niamini tu na kukubali mafunzo ya dini yetu.  Nikifundishwa kuwa    kuwasiliana na mungu ni kuepukana na njia za kutafakari sana huku nikiamini kuwa mungu mmoja hasa yupo na ninaweza kuzungumza nae na kwamba ananisikia.


Fikra zangu zilivyopanuka


Nilipotimia miaka 13 familia yangu ikaja kuishi Canada kuwa pamoja na baba yangu.   Ghafula nikajikuta kwenye mawingu ya mabadiliko  ya maadili .  Ikanichukua muda kujisawazisha.    Maisha yangu nyumbani yalikuwa ya kubanwa kabisa wakikhofu wazazi wangu nisibadilike kuingia katika  maadili na kuathirika na tamaduni za nchi hii.  Nilipoingia chuo kikuu nikajihisi huru kidogo na ndipo nikaanza kuwaza vile nilivyo kuwa nahisi undani mwangu.  Nilisoma masomo ya Biology, Chemistry na Physics nikitaka niwe Engineer, ili tu niwafurahishe wazazi wangu waliokosa mtoto wa kiume, kwani hiyo ilikuwa ni tamanio lao kubwa na   baba yangu hakunipa mapenzi yale anayostahiki baba kumpa mwanawe.  Na tamanio hili lilikuwa likiwavunja moyo katika mujtamaa wetu kuwa hawana mtoto wa kiume bila ya kufikiri kuwa hayo ni makadirio ya Mungu. 


Nilipokuwa naingia ndani kabisa katika masomo ya Biology na kuelimika elimu ya mwili wa binaadamu, nilikuwa nikiwaza uzuri, ufundi, ustadi na uhodari wa maumbile haya, kwamba kila sehemu ya mwili ina kazi yake maalumu na zote zinafanya kazi barabara kabisa kumuezesha binaadamu aishi.   Je!  Ni nani huyo aliyetengeneza mjengo huu wa mwili?   Yuko wapi?  Akili yangu ikawa inanizunguka sana!! Nikitazama mbingu na ardhi, jua, mwezi, mimea, wanyama na bahari, almuradi nilitembea mbali kwa mawazo na kuwaza mjenzi wa hayo yote bila ya kumjua ni nani, huku sina raha kabisa na hamu kubwa imenishika nimtambue. 


Ibada na ada yangu zikaanza kuwa hazina muhimu akilini mwangu, nikaanza kuzikataa ndani ya moyo wangu kwanza.   Nikaanza kuwaza sababu ya maisha yetu binaadamu.  Nikahisi kuwa kuna kitu kilichopunguka katika kufahamu kwangu kuhusu maisha. Vipi Muumba wa binaadamu na dunia yote hakujijulisha kwetu?   



Kuumwa kwangu


Ikaendelea hivyo mpaka siku za Spring 2002, nikaanza kuumwa.  Sikuwa na wasiwasi sana nikajua   kuwa nitapona tu na kila kitu kitarudi kama mwanzo. Lakini haikuwa hivyo, nilizidi kuumwa mpaka nikafikia katika hali ya kukata tamaa ya maisha, niliona ndio basi nakufa, hakuna wa kunisaidia, sio daktari wala mama, wala ndugu wala rafiki, wote hawakuweza kunifaa hata mimi mwenyewe sikuweza kujisadia lolote.    Niliyatamani hayo mauti na kupendelea bora nife kuliko kuadhibika na mateso hayo ya maumivu.  Nikawa najiuliza, "Kama mungu anadhibiti mambo yote ya watu vipi ananitesa hivi? Kama kweli yupo mbona haniponyeshi na wazee wangu wanamuomba?
Nikatambua kuwa uzuri wangu, uhodari wangu, ujeuri na kiburi changu, vyote nilokuwa navyo vikawa vinayayuka, sina tena hayo, kwani faida gani kuwa nayo hayo na hayanifai kitu katika hali hii?   Maumivu makali, mateso, dhiki ya roho, kuchanganyikwa akili kulinipeleka kuwa katika kiza,  nikawa sioni sisikii, nimo matesoni tu na tamaa ya  kuishi inazidi kupotea. 




Kuzungmza na Mungu na kusikia kuhusu Uislamu


Kwa mara ya kwanza nikaanza kuzungumza na Mungu na kumuomba, bali kumuomba msamaha na kusema, "Ewe Mungu kama kweli upo, na nafikiri kweli upo, basi nisamehe, nisaidie na nionyeshe njia, na nijulishe sababu ya maisha na ukweli wake”.  Baada ya haya, kidogo nikahisi raha fulani imepenya katika moyo wangu. 

Siku ya pili yake nilikuwa natizama T.V., walikuwa wakionyesha kisa cha mtu aliyesilimu.  Nilipendezewa na mabadiliko aliyopata huyo mtu baada ya kuingia katika Uislamu, zaidi katika utakaso, ukweli, uaminifu, udhalilifu wake yalikuwa ni mambo ya tunu kabisa.   Alikiri huyo mtu kuwa Uislamu ndio uliomfanya kupata sifa hizo.   Nikasema moyoni "Lazima niitafute hii dini ya Kiislamu niisome niijue ikoje?  Waislamu wanaamini nini kuhusu Mungu? Hili ni wazo kubwa muhimu nililotaka kujua jibu lake.

Nikaanza kutafuta katika internet kuhusu Uislamu nikasoma Tauhiid na iliniingia moja kwa moja akilini na kuikubali, maana niliona yote yaliosemwa yalikuwa ya hikma na yenye kuleta maana kabisa.  Zaidi kilichonivutia ni kukazaniwa neno la " Laa Ilaaha Illa Allaah” nikawa nawaza haya sana bila ya kiasi. Nikaanza kujifundisha tabia za Kiislamu nikapendezewa kuona sifa nzuri nzuri na mafundisho yake.  Nikawaza sasa, "Je vipi kuamini kwao kuhusu akhera?  Wanaamini nini baada ya mtu kufa?”    Nikaanza kusoma tafsiir ya Qur’an nikatambua kuwa kweli haya ni maneno ya Mungu hasa niliyekuwa namtafuta.  Ni kitabu cha mwisho, kilichokamilika na risala na uongofu wa Muumba uliomo humo, haukuwa na shaka ulikuwa wa wazi kabisa na wa kuridhisha.    Huku nikipata nafuu ya maumivu. 

Mama yangu akawa anaona tofauti yangu ya siha na pia akaona mabadiliko ya tamaa yangu, na kuwa ipo furaha fulani inayoonekana katika uso wangu.  Nikawa namuonyesha maneno ya Allaah akawa anayapokea vizuri na kukubaliana na mimi (huku sijui matokeo yake yatakuwa nini baada kuingia Uislamu). Qur'an ikanizidisha kuwaza dalili za Mungu  zikawa zinakubaliana kabisa na mawazo yangu ya mwanzo hasa nikipitia katika aya kama hizi:

 إِنَّ فِي خَلْقِ السَّمَاوَاتِ وَالأَرْضِ وَاخْتِلاَفِ اللَّيْلِ وَالنَّهَارِ وَالْفُلْكِ الَّتِي تَجْرِي فِي الْبَحْرِ بِمَا يَنفَعُ النَّاسَ وَمَا أَنزَلَ اللّهُ مِنَ السَّمَاءِ مِن مَّاء فَأَحْيَا بِهِ الأرْضَ بَعْدَ مَوْتِهَا وَبَثَّ فِيهَا مِن كُلِّ دَآبَّةٍ وَتَصْرِيفِ الرِّيَاحِ وَالسَّحَابِ الْمُسَخِّرِ بَيْنَ السَّمَاء وَالأَرْضِ لآيَاتٍ لِّقَوْمٍ يَعْقِلُونَ   



{Hakika katika kuumbwa kwa mbingu na ardhi, na kukhitalifiana usiku na mchana, na marikebu ambazo hupita baharini kwa viwafaavyo watu, na maji anayo yateremsha Mwenyezi Mungu kutoka mbinguni, na kwa hayo akaihuisha ardhi baada ya kufa kwake, na akaeneza humo kila aina ya wanyama; na katika mabadiliko ya pepo, na mawingu yanayo amrishwa kupita baina ya mbingu na ardhi, bila shaka zimo Ishara kwa watu wanao zingatia}  Al Baqara 2.164 

 Nikazidi kujua aya zinazoelezea maumbile ya ulimwengu na binaadamu, elimu ambayo imejulikana na binaadamu baada ya miaka ya utafiti wa elimu ya sayansi.

 أَوَلَمْ يَرَ الَّذِينَ كَفَرُوا أَنَّ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضَ كَانَتَا رَتْقاً فَفَتَقْنَاهُمَا وَجَعَلْنَا مِنَ الْمَاء كُلَّ شَيْءٍ حَيٍّ أَفَلَا يُؤْمِنُونَ    



{Je! Hao walio kufuru hawakuona kwamba mbingu na ardhi zilikuwa zimeambatana, kisha Sisi tukazibabandua? Na tukajaalia kwa maji kila kilicho hai? Basi je, hawaamini?}   Anbiyaa 21:30

  ثُمَّ اسْتَوَى إِلَى السَّمَاء وَهِيَ دُخَانٌ فَقَالَ لَهَا وَلِلْأَرْضِ اِئْتِيَا طَوْعاً أَوْ كَرْهاً قَالَتَا أَتَيْنَا طَائِعِينَ    



{Kisha akazielekea mbingu, na zilikuwa moshi, akaziambia hizo na ardhi: Njooni, kwa khiari au kwa nguvu! Vyote viwili vikasema: Tumekuja nasi ni wat'iifu} Ha Meem Fussilaat 41:11

  وَالسَّمَاء بَنَيْنَاهَا بِأَيْدٍ وَإِنَّا لَمُوسِعُونَ   



{Na mbingu tumezifanya kwa nguvu na uwezo na hakika Sisi bila ya shaka ndio twenye uwezo wa kuzitanua}  Adhariyaat  51:47

وَاللَّهُ خَلَقَ كُلَّ دَابَّةٍ مِن مَّاء فَمِنْهُم مَّن يَمْشِي عَلَى بَطْنِهِ وَمِنْهُم مَّن يَمْشِي عَلَى رِجْلَيْنِ وَمِنْهُم مَّن يَمْشِي عَلَى أَرْبَعٍ يَخْلُقُ اللَّهُ مَا يَشَاءُ إِنَّ اللَّهَ عَلَى كُلِّ شَيْءٍ قَدِيرٌ   


{Na Mwenyezi Mungu ameumba kila kinyama kutokana na maji. Wengine katika wao huenda kwa matumbo yao, na wengine huenda kwa miguu miwili, na wengine huenda kwa miguu mine. Mwenyezi Mungu huumba ayatakayo. Hakika Mwenyezi Mungu ni Muweza wa kila kitu.}  An-Nuur 24:45

Haya hayawezi kuwa ni maneno ya binaadamu.     Nikaamini kabisa maneno haya kuwa hakika ni maneno ya pekee ya Muumba.   Sasa vipi basi binaadamu wote hawatambui haya?  Vipi hawamtambui Mungu wao Aliyewaumba?  Nikazidi kupitia aya kama hizi zinazotaja kuhusu Mungu Muumba, na kuzidi kutumainika na dini ya Kiislamu.

قُلْ مَن يَرْزُقُكُم مِّنَ السَّمَاءِ وَالأَرْضِ أَمَّن يَمْلِكُ السَّمْعَ والأَبْصَارَ وَمَن يُخْرِجُ الْحَيَّ مِنَ الْمَيِّتِ وَيُخْرِجُ الْمَيَّتَ مِنَ الْحَيِّ وَمَن يُدَبِّرُ الأَمْرَ فَسَيَقُولُونَ اللّهُ فَقُلْ أَفَلاَ تَتَّقُونَ  


{Sema: Ni nani anaye kuruzukuni kutoka mbinguni na kwenye ardhi? Au ni nani anaye miliki kusikia na kuona? Na nani amtoaye hai kutoka maiti, na akamtoa maiti kutoka aliye hai? Na nani anaye yadabiri mambo yote? Watasema: Allah, Mwenyezi Mungu. Basi sema: Je! Hamchi? }

 فَذَلِكُمُ اللّهُ رَبُّكُمُ الْحَقُّ فَمَاذَا بَعْدَ الْحَقِّ إِلاَّ الضَّلاَلُ فَأَنَّى تُصْرَفُونَ   


 [Basi huyo ndiye Mwenyezi Mungu, Mola Mlezi wenu wa haki. Na kipo kitu gani baada ya haki, isipokuwa upotovu tu? Basi huwaje mkageuzwa?} 


 كَذَلِكَ حَقَّتْ كَلِمَتُ رَبِّكَ عَلَى الَّذِينَ فَسَقُواْ أَنَّهُمْ لاَ يُؤْمِنُونَ   



{Ndio kama hivyo kauli ya Mola wako Mlezi itakavyo wathibitikia wale walio potoka, ya kwamba hawatoamini.}

 قُلْ هَلْ مِن شُرَكَآئِكُم مَّن يَبْدَأُ الْخَلْقَ ثُمَّ يُعِيدُهُ قُلِ اللّهُ يَبْدَأُ الْخَلْقَ ثُمَّ يُعِيدُهُ فَأَنَّى تُؤْفَكُونَ   


{Sema: Je! Yupo katika miungu yenu ya ushirikina aliye anzisha kuumba viumbe, na kisha akavirejesha? Huwaje, basi, mkadanganywa?]

قُلْ هَلْ مِن شُرَكَآئِكُم مَّن يَهْدِي إِلَى الْحَقِّ قُلِ اللّهُ يَهْدِي لِلْحَقِّ أَفَمَن يَهْدِي إِلَى الْحَقِّ أَحَقُّ أَن يُتَّبَعَ أَمَّن لاَّ يَهِدِّيَ إِلاَّ أَن يُهْدَى فَمَا لَكُمْ كَيْفَ تَحْكُمُونَ   


{Sema: Je! Yupo katika miungu yenu ya ushirikina anaye ongoa kwendea Haki? Sema: Mwenyezi Mungu anaongoa kwendea Haki. Basi, je, anaye stahiki kufuatwa ni yule Mwenye kuongoa kwendea Haki au asiye ongoa ila aongozwe yeye? Basi nyinyi mna nini? Mnahukumu namna gani?}Yunus   10: 31 – 35

Huu ndio uongofu niliokuwa nautafuta!  Furaha ikanizidi ya moyo na kujihisi mwepesi kabisa. Qur'aan hii haikunionyesha uongofu tu, bali imenionyesha uvumbuzi wa matatizo ya binaadamu akiwa pekee au akiwa pamoja na familia yake au akiwa   na mujtamaa wake  (jamaa)  .  Imemuonyesha wazi binaadamu wajibu wake, haki yake na jukumu lake katika madaraka yake.  Imempangia maisha katika mambo ya mahitajio yake, tabia na matendo yake katika jamii kwa njia iliyo ya hikma na ya heshima kabisa. 

Qur'ani imefundisha binaadamu vipi kujiepusha na matamanio ya nafsi yaliyo kuwa ya mazowea katika nyoyo za binaadamu mwanamme na mwanamke.

وَقُل لِّلْمُؤْمِنَاتِ يَغْضُضْنَ مِنْ أَبْصَارِهِنَّ وَيَحْفَظْنَ فُرُوجَهُنَّ وَلَا يُبْدِينَ زِينَتَهُنَّ إِلَّا مَا ظَهَرَ مِنْهَا وَلْيَضْرِبْنَ بِخُمُرِهِنَّ عَلَى جُيُوبِهِنَّ وَلَا يُبْدِينَ زِينَتَهُنَّ إِلَّا لِبُعُولَتِهِنَّ أَوْ آبَائِهِنَّ أَوْ آبَاء بُعُولَتِهِنَّ أَوْ أَبْنَائِهِنَّ أَوْ أَبْنَاء بُعُولَتِهِنَّ أَوْ إِخْوَانِهِنَّ أَوْ بَنِي إِخْوَانِهِنَّ أَوْ بَنِي أَخَوَاتِهِنَّ أَوْ نِسَائِهِنَّ أَوْ مَا مَلَكَتْ أَيْمَانُهُنَّ أَوِ التَّابِعِينَ غَيْرِ أُوْلِي الْإِرْبَةِ مِنَ الرِّجَالِ أَوِ الطِّفْلِ الَّذِينَ لَمْ يَظْهَرُوا عَلَى عَوْرَاتِ النِّسَاء وَلَا يَضْرِبْنَ بِأَرْجُلِهِنَّ لِيُعْلَمَ مَا يُخْفِينَ مِن زِينَتِهِنَّ وَتُوبُوا إِلَى اللَّهِ جَمِيعاً أَيُّهَا الْمُؤْمِنُونَ لَعَلَّكُمْ تُفْلِحُونَ 


{Na waambie Waumini wanawake wainamishe macho yao, na wazilinde tupu zao, wala wasionyeshe uzuri wao isipo kuwa unao dhihirika. Na waangushe shungi zao juu ya vifua vyao, wala wasionyeshe uzuri wao ila kwa waume zao, au baba zao, au baba wa waume zao, au watoto wao, au watoto wa waume zao, au kaka zao, au wana wa kaka zao, au wana wa dada zao, au wanawake wenzao, au iliyo wamiliki mikono yao ya kuume, au wafwasi wanaume wasio na matamanio, au watoto ambao hawajajua mambo yaliyo khusu uke. Wala wasipige chini miguu yao ili yajuulikane mapambo waliyo yaficha. Na tubuni nyote kwa Mwenyezi Mungu, enyi Waumini, ili mpate kufanikiwa}  An Nuur   24:  31

يَا أَيُّهَا النَّبِيُّ قُل لِّأَزْوَاجِكَ وَبَنَاتِكَ وَنِسَاء الْمُؤْمِنِينَ يُدْنِينَ عَلَيْهِنَّ مِن جَلَابِيبِهِنَّ ذَلِكَ أَدْنَى أَن يُعْرَفْنَ فَلَا يُؤْذَيْنَ وَكَانَ اللَّهُ غَفُوراً رَّحِيماً   


{Ewe Nabii! Waambie wake zako, na binti zako, na wake za Waumini wajiteremshie nguo zao. Hivyo ni karibu zaidi kuweza kutambulikana wasiudhiwe. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye kusamehe, Mwenye kurehemu.}  Ahzaab 33:59


Qur'aan imempa haki mwanamke kwa kulinganisha na uumbile lake na hali kadhalika mwanamme.  Uislamu ni mpango mkamilifu na njia ya maisha bora kabisa ya kumfaa binaadamu kumuongoza katika mwangaza, kumtoharisha na maovu, na kumtoa katika kiza na kumuweka katika heshima anayostahiki,  nimetambua kuwa ni hiari yake mtu kufuata haki au kuikanusha.  

 وَلَا تَزِرُ وَازِرَةٌ وِزْرَ أُخْرَى وَإِن تَدْعُ مُثْقَلَةٌ إِلَى حِمْلِهَا لَا يُحْمَلْ مِنْهُ شَيْءٌ وَلَوْ كَانَ ذَا قُرْبَى إِنَّمَا تُنذِرُ الَّذِينَ يَخْشَوْنَ رَبَّهُم بِالغَيْبِ وَأَقَامُوا الصَّلَاةَ وَمَن تَزَكَّى فَإِنَّمَا يَتَزَكَّى لِنَفْسِهِ وَإِلَى اللَّهِ الْمَصِيرُ   

وَمَا يَسْتَوِي الْأَعْمَى وَالْبَصِيرُ   


وَلَا الظُّلُمَاتُ وَلَا النُّورُ   


وَلَا الظِّلُّ وَلَا الْحَرُورُ   


وَمَا يَسْتَوِي الْأَحْيَاء وَلَا الْأَمْوَاتُ إِنَّ اللَّهَ يُسْمِعُ مَن يَشَاءُ وَمَا أَنتَ بِمُسْمِعٍ مَّن فِي الْقُبُورِ   


{Na mbebaji habebi mzigo wa mwingine. Na aliye topewa na mzigo wake akiomba uchukuliwe hautachukuliwa hata kidogo, na angamwomba jamaa yake. Hakika wewe unawaonya wale wanao mcha Mola wao Mlezi kwa ghaibu, na wanashika Sala. Na anaye jitakasa, basi anajitakasa kwa ajili ya nafsi yake. Na marejeo ni kwa Mwenyezi Mungu } 

{Na kipofu na mwenye kuona hawalingani.}

{Wala giza na mwangaza}  

{Wala kivuli na joto}

{Wala hawalingani walio hai na maiti. Hakika Mwenyezi Mungu humsikilizisha amtakaye. Wala wewe si wa kuwasikilizisha walio makaburini.} Fatir   35:  18 -22

أَوَ مَن كَانَ مَيْتاً فَأَحْيَيْنَاهُ وَجَعَلْنَا لَهُ نُوراً يَمْشِي بِهِ فِي النَّاسِ كَمَن مَّثَلُهُ فِي الظُّلُمَاتِ لَيْسَ بِخَارِجٍ مِّنْهَا كَذَلِكَ زُيِّنَ لِلْكَافِرِينَ مَا كَانُواْ يَعْمَلُونَ   

{Je, aliye kuwa maiti kisha tukamhuisha, na tukamjaalia nuru inakwenda naye mbele za watu, mfano wake ni kama aliyoko gizani akawa hata hawezi kutoka humo? Kama hivyo makafiri wamepambiwa waliyo kuwa wakiyafanya}    An-Aam  6:122


Kuchukua Shahada (kuingia Uislamu)


Aya zote hizo na nyingine nyingi zikanifanya nikubali Uislamu ndani ya moyo wangu japokuwa sijakiri Shahada.  Nikaamua sasa nikatafute Muislamu anipe shahada.  Nani atakaenipa? Wapi?  Nikachukua kitabu cha simu kutafuta duka la vitabu vya KiiIslamu.  Nikapiga simu duka moja nikafunga safari kulifuata, nalo ni mbali na kwetu.  Kufika nikajidai kwanza kutizama vitabu kisha kumuuliza mwenye duka kuhusu Uislamu na vipi kuingia katika dini hii, akanifahamu kuwa nataka kuchukua shahada. Akaniuliza, "Je ndugu unataka kuchukua shahada hivi sasa?"  Machozi ya furaha yakanitoka na kumuitikia, hapo hapo nikakiri shahada, "Ash-hadu An-Laa Ilaaha Illa Allaah Wa Ash-hadu Anna Muhammadan Rasulu Allaah.” 

Furaha ilioje moyoni mwangu, nilijihisi ni mtu mwingine kabisa.  Nikarudi nyumbani huku natabasamu, furaha ikidhihirika usoni mwangu.  Zikapita siku nikawa najifunza kuswali na kuibia kuswali kwani niliogopa wazazi wasijue, ambao nimekuja kujua kuwa jamii yetu ni maadui wakubwa   wa Uislamu.  Nikaendelea kuficha, lakini mama yangu alikuwa hana raha kuniona kutwa niko kwenye internet nikisoma mambo ya Kiislamu, mwisho ikabidi nimwambie.   Kwa vile aliniona kuwa nimekuwa mtu mwenye furaha, na bado sijapona vizuri, ikawa kama kuumwa kwangu ni usalama wa kuingia dini hii.  Kama kwamba nikimsoma mawazo yake mama yangu anasema, "Si kitu madamu unapata nafuu ya  maradhi yako na madamu una furaha basi, lakini naichukia hiyo dini,” kwani alikwisha niambia kuwa utatutia aibu kubwa katika jamii yetu, tutakuwa na uso gani mbele ya jamaa zetu?  

Ikawa kila siku ni masuali hayo hayo, na habari zikawafikia jamaa zangu wa ki Singa Singa ambao hawakunyamaza, bali waliwaita wazazi wangu na kuwataka watoke katika aibu hiyo.  Wazee wangu hawakuweza kunilazimisha kwani walihofu nisirudie hali yangu ya kuumwa. Subhana Allaah! Nikawa nasema moyoni kila kitu kina kheri yake, kuumwa kwangu kumekuwa kheri kwangu kwamba wazazi wangu wananistahmilia kubadili dini yangu ingawa wanaichukia .  Ukhasama ukawa baina ya jamii yangu na wazazi wangu.  Wakaukata uhusiano kabisa, na wachache tu ndio waliobakia kuwa na aila yangu.  Jeuri, kiburi na chuki ya dini ya Kiislamu ndio sababu ya ari yao hiyo.    

Nikaanza kwenda msikitini nikajuana na wanawake wengi walionipokea kwa mapenzi na undugu wa dhati wa Kiislamu.  Nikajulishwa na mwalimu wa Qur'ani nikawa nakwenda kwake kusoma.  Mwalimu huyo ni kama mama yangu,  dada yangu,   rafiki yangu, nikashikana  naye sana, alikuwa akinisaidia kwa kila aina ya njia ya kuimarisha dini yangu.   Nikajifunza namna ya kusoma Qur'aani (Qaida) na Alhamdulillah nikaweza kusoma na kuijua vizuri vile inavyopasa.

Baada ya siku chache kuanza kujifunza Qur'ani, nilimuota bibi yangu mzaa mama ambaye tokea kufariki kwake miaka mingi sikupata kumuota.  Nilimuota anafuraha na huku anamkumbatia mwalimu wangu.  Ndoto ilikuwa ya wazi kabisa hata niliamka usingizini na kupigwa na bumbuwazi!  Ni ndoto au ni kweli?  Ni ndoto! Ndoto ya kweli!  Bibi yangu amefurahi mimi kuingia katika uislamu!  Bibi yangu ananijulisha kuwa niko katika njia ya haki.  Jambo la mwanzo nilipoamka nikamuelezea mama yangu ambaye naye alishangaa, lakini akanipuuza kwa vile hakutaka niiamini hii dini yangu.  
  
Wazee wangu wakawa wanatia shaka na mimi kutoka kwangu kwingi kuhudhuria darasa, mikutano ya dini, na hata mara nyingine wakinitumia mtu kunifuata kuniona nakwenda wapi.  Ajabu ni kwamba nilipokuwa natoka kwenda disco, na sinema na kurudi usiku hapo mwanzoni walikuwa hawaniambii kitu.  Lakini nnapokwenda kusoma dini na kurudi mapema nyumbani kuweko chumbani kwangu wakiniambia, "mbona kutwa uko chumbani hutoki?”  Maajabu!!

Nikaendelea hivyo hivyo na huku nikizidi kupata nafuu ingawa sikupona kabisa, lakini Alhamdulillah namshukuru Allaah سبحانه وتعالى Kunifikisha hapa nilipofikia kwa Kuniongoza, Kunitoa katika kiza na Kunitia katika mwangaza. Na ndio maana nimejibadilisha jina langu kujiita 'Nuur' badili ya  Rimmie.   Alhamdulillah, neema zote ni Zake Mola wa Mbingu na Ardhi namuomba Allaah سبحانه وتعالى  Azidi Kuithibitisha imani yangu na Anijaaliye miongoni mwa watu wema mpaka nitakapokutana Naye.
Amiin.


Maelezo zaidi  kutoka kwa mwalimu wake Nuur


Aliponipigia simu Nuur kwa mara ya kwanza kutaka kusoma Qur'ani, na nilipojua kuwa katoka katika jamii ya Singa Singa, kwanza mwili ulinisisimka, maana  niliona wengi wao wanaobadili ni  kutoka dini ya Ukristo na kutoka jamii nyingine lakini sijapatapo kuona kutoka jamii hii. Nilikuwa na hamu kubwa ya siku tulioagana ifike.  Nikachungulia dirishani kumsubiri wakati anakuja na nilipomuona, Subhana Allaah, msichana mwenye uzuri wa kupendeza kabisa, mpole, na juu ya hayo nimeona ajabu ya akili yake aliyomjaalia Allaah سبحانه وتعال.  Alikuwa akihudhuria mara mbili tu kwa wiki, kila mara akitumia saa moja na nusu,  akisoma masomo mawili au matatu kwa mara moja, kisha  baada ya siku   ya pili yake akirudi amekwishajifunza vizuri, hata ameweza kumaliza kujifunza kusoma Qaida ya Qur'aan kwa muda wa miezi miwili na nusu tu! Kisha akawa anaendelea kusoma sura mpaka akafikia karibu kumaliza juzuu ya Amma nzima.  Maajabu ni kwamba hata  matamshi yake ya kiarabu yalikuwa kama mtu aliyezaliwa nayo lugha ya Kiarabu.  Na hawa ndio wale Allaah سبحانه وتعالى Kawataja kuwa 'Ulul-Al-baab" yaani "Watu wenye akili.”  (Ya kutafakari )

Siku ya harusi yake  iliofanywa msikitini, alipendeza sana,  na ajabu ni kuwa hakujipamba mapambo yeyote, si wanja, wala  podari wala si rangi ya mdomo,   lakini alikuwa ananġaa kwa uzuri na ucheshi,  Nuru ya kweli ilikuwa ikinġara usoni mwake.    Mama yake alikuwa akilia sana.  Nikamwambia "Nuur! mama yako analia sana"  Akanijibu  "ewe dada yangu, huonii kuwa analia machozi ya kusikitika  kwamba siku ya leo hakutegemea kumuozesha mwanawe msikiti wa Waislamu?  na siyo machozi ya furaha wakati mimi nna furaha ya kupata dini ya haki?  Basi mwache alie tu,  machozi hayo kwangu hayana thamani, namuomba tu  Allaah سبحانه وتعالى Amuongoze   na yeye".      

Hivi sasa Nuru anasoma masomo ya Sheria ya Kiislamu, aliniambia kuwa anataka kujua lugha ya Kiarabu vizuri ili aweze kufanya daawa katika jamii yake ya Kipanjabi. 

Kwa vile ni nadra kuingia katika Uislamu   mtu kutoka kwenye jamii hiyo na kwa jinsi ilivyothibitika imani yake huyu msichana, nimependa kukiita kisa chake "Wardi katika msitu"    "A rose in the forest".

Tumuombe  Allaah سبحانه وتعالى Athibitishe imani yake na zetu sote.  Amiin. 



FROM: www.alhidaaya.com

Post a Comment

0 Comments