ads

MKATABA WA HUDAYBIYA


BISMILLAH RAHMANI RAHIM

  
     Abubakar (Radhiya Allaahu ‘anhu) alikua akimfahamu na akimuelewa vizuri sahibu yake (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam)kupita Masahaba wote (Radhiya Allaahu ‘anhu), na alikuwa na uhakika kuwa yote anayoyasema ni Wahyi utokao kwa Mola wake Subhanahu wa Taala.
        Katika mwaka wa tano baada ya kuhamia Madina, Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam)pamoja na Masahaba wake (Radhiya Allaahu ‘anhu) waliondoka Madina kuelekea Makkah kwa nia ya kufanya Umra. Wakapiga kambi karibu na mji wa Makkah mahali panapoitwa Al Hudaibiyya, kisha wakamtuma Othman bin Affan (Radhiya Allaahu ‘anhum) ende Makkah kuwajulisha Makureshi juu ya nia yao hiyo na kwamba hawakuja kwa nia ya kupigana vita.
         Makureshi wakapeleka majeshi yao kutaka kuwazuia, na baada ya majadiliano marefu yaliyopita baina yao, wakaamua kumtuma mjumbe wao aitwaye Suhail bin Amr, aliyeweza kufikia makubaliano na Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam), yaliyokuja kujulikana kwa jina la Makubaliano ya Al Hudaibiyya.

Yafuatayo ni baadhi ya shuruti za makubaliano hayo;

· Waislamu warudi Madina mwaka huu na wafanye Umra mwaka ufuatao.
· Waislamu wanalazimika kumrudisha kwa Makureish yoyote atakayeingia katika dini yao na kukimbilia Madina, lakini Makureshi hawalazimiki kumrudisha atakayetoka katika Uislamu na kukimbilia Makkah.
· Wasipigane vita kwa muda wa miaka kumi, na wawe wanaendeana watakavyo.
         Kabla ya mkataba huo kutiwa sahihi (saini), Waislamu walistukia kijana mmoja aitwae Aba Jandal aliyesilimu lakini alikuwa akiishi Makkah akipitishwa mbele yao akiwa amefungwa minyororo shingoni huku na kubebeshwa jiwe kubwa akipiga kelele akiwaomba Waislamu wenzake wamuokoe kutokana na adhabu hiyo.
Kijana huyu Aba Jandal ni mwana wa Suhail, mjumbe wa Makureish katika sulhu hiyo.
          Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam), alimuonea huruma kijana huyo, akamtaka Suhail amruhusu wamchukuwe kwa sababu mkataba ulikuwa bado haukutiwa saini wala haukupigwa mhuri, lakini baba yake alikataa na kutishia kuuvunja mkataba na kuanzisha vita ikiwa watajaribu kumchukua kwa nguvu.
Abu Jandal alikuwa akipiga kelele huku akisema;
"Enyi Waislamu wenzangu! mnaniacha nirudi kwa washirikina hawa na mimi nataka himaya yenu?"
Mtume(Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) akamwambia ;
"Kuwa na subira, na Mwenyezi Mungu atakujaalia utoke katika janga hilo".
Omar bin Khattab (Radhiya Allaahu ‘anhu) hakuweza kuyastahamilia haya, akamuendea Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam)na kumuuliza;
"Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, wewe si Mtume wa Haki?"
Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam)akamjibu;
"Ndiyo, ewe Omar".
Akauliza tena;
" Kwa nini basi tunakubali kujidhalilisha?"
Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam)akamwambia;
"Ewe Omar, mimi ni Mtume wa Mwenyezi Mungu, siwezi kumuasi, na Yeye ndiye atakayetunusuru".
Omar (Radhiya Allaahu ‘anhu) akauliza;
"Si ulituahidi kuwa tutakwenda Makkah na tutatufu katika nyumba kongwe?"
Mtume(Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam)akajibu;
"Nilikwambia kuwa ni mwaka huu ewe Omar?"
Omar akajibu;
"La hukusema hivyo."
Mtume(Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam)akasema;
"Utakwenda Makkah ewe Omar na utatufu penye nyumba."
Omar pamoja na baadhi ya Masahaba (Radhiya Allaahu 'anhum) hawakuridhika na baadhi ya masharti yaliyokuwemo ndani ya mkataba ule, wao waliona kuwa Waislamu wamekubali kujidhalilisha kwa kuyakubali masharti yote ya makafiri, na hii ni kwa sababu dhahiri yake mkataba huo si mzuri juu ya Waislamu, lakini kwa anayeona mbali mkataba huo ulikuwa ni ufunguzi mkubwa kwa Waislamu, kama alivyosema Mwenyezi Mungu katika Suratul Fat-h aya ya mwanzo;
"Bila shaka tumekwishakupa kushinda kuliko dhahiri"
Mwenyezi Mungu katika aya hii anatujulisha kuwa kuukubali mkataba huo ni ushindi mkubwa kwa Waislamu, juu ya kuwa dhahiri yake ni kukubali masharti yote ya makafiri, na hii ni inatokana na sababu zifuatazo;
1) Kutokana na suluhu hiyo, makafiri walifungika wasiweze kupigana vita dhidi ya Waislamu muda wa miaka Kumi.
2) Katika muda wote huo Waislmu wakawa na uwezo wa kujishughulisha na kuieneza dini yao miongoni mwa makabila mengine ya Bara arabu, pamoja na nchi za Sham.
3) Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam)alituma ujumbe kwa wafalme mbali mbali
4) Wale waliosilimu wasioruhusiwa kukimbilia Madina kwa ndugu zao Waislamu, ni bora kwao kubaki Makkah kwa ajili ya kuwalingania watu katika dini ya Kiislam huko Makkah.
5) Makafiri watakaorudi Makkah iwapo watatoka katika Uislam, hawataudhuru Uislam.
        Sababu hizi na nyinginezo ambazo si wasaa wake huu kuzitaja ni dalili kuwa mkataba huo undani wake ulikuwa na manufaa makubwa kwa Waislamu, juu ya kuwa dhahiri yake ni kusalimu amri na kukubali masharti yote ya Makureshi.
Na hii ndiyo sababu iliyomfanya Omar (Radhiya Allaahu ‘anhu) asiridhike nao, wala asisimame hapo. Kwani alimwendea pia Abubakar Al Siddiq (Radhiya Allaahu ‘anhu) na kumuuliza tena masuali yale yale;
"Ewe Abubakar, Muhammad si Mtume wa Haki?"
Abubakar (Radhiya Allaahu ‘anhu); "Ndiyo"
Omar (Radhiya Allaahu ‘anhu); "Tukipambana nao makafiri hawa, si atakayekufa upande wetu ataingia Peponi na wao wanaingia Motoni?"
Abubakar (Radhiya Allaahu ‘anhu); "Ndiyo".
Omar (Radhiya Allaahu ‘anhu); "Kwa nini basi tunakubali kujidhalilisha?"
Abubakar (Radhiya Allaahu ‘anhu);
"Ewe Omar, yeye ni Mtume wa Mwenyezi Mungu na hawezi kumuasi, na Mwenyezi Mungu ndiye atakayemnusuru, kamatana naye kwani Wallahi yupo katika Haki".
Majibu yale yale ya Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam)kayapata kwa Abubakar (Radhiya Allaahu ‘anhu), na Mwenyezi Mungu akawateremshia Waislamu utulivu nyoyoni mwao.
Mwenyezi Mungu anasema;
"Yeye ndiye aliyeteremsha utulivu katika nyoyo za Waislamu ili waongezeke imani juu ya imani yao".
Suratul Fat-h 4
Omar(Radhiya Allaahu ‘anhu) alisema baadaye;
"Nikatambua kuwa ile ndiyo Haki".
       Mwaka wa tisa Hijri ndio mwaka ulioitwa 'Mwaka wa Wajumbe' na hii ni kutokana na wajumbe wa makabila mbali mbali ya kiarabu waliokuja kusilimu mbele ya Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam).

WABILLAH TAUFIQ

Post a Comment

2 Comments